Jeshi la Polisi kanda maalum ya Dar Es Salaam leo limefanikiwa kumkamata askari bandia akiwa amevaa Sare za Jeshi la Polisi kitengo cha usalama barabarani.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Kamishina wa Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, DCP Suleiman Kova amesema leo majira ya saa moja na nusu asubuhi wamefanikiwa kumkamata James Hussen mwenye umri wa miaka 45 mkazi wa Kimara Tangi Bovu akiwa amevaa sare hizo huku akiendelea na utapeli wa kujifanya askari wa kitengo cha usalama barabarani.

Aidha Kamanda Kova ametoa wito kwa wananchi kutoa taarifa kwa jeshi la polisi mara wanapomtilia mashaka askari yeyote na pia kuwaomba wananchi wasikubali kupigwa bao bali kuwataka askari kwenda nao kituo cha polisi pindi wanapokamatwa na makosa.