MAGAZETI YA SIKU

 Waafrika waongeza kasi kuwekeza barani Afrika
 
Wakati vuguvugu la gesi iliyogunduliwa mkoani Mtwara lilipokuwa likiendelea, Waziri Mkuu Mizengo Pinda alikuwa akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa kiwanda cha saruji kinachomilikiwa na Rais na Ofisa Mkuu Mtendaji wa Dangote Group, Alhaji Aliko Dangote.
Dangote ambaye ni bilionea amewekeza karibu Dola 500 milioni za Marekani sawa na Sh8 tilioni katika kiwanda hicho kitakachojengwa mkoani Mtwara.
Kiwanda cha Dangote kinatarajiwa kuzalisha tani milioni 3 za saruji kwa mwaka sawa na mifuko 150,000 kwa siku yenye uzito wa kilogramu 50 na kutengeneza ajira za kudumu 1,000 na zisizo rasmi 9,000.
Mbali na Tanzania, Dangote amewekeza pia katika nchi nyingine 14 barani Afrika katika uzalishaji wa bidhaa hiyo muhimu katika ujenzi wa miundombinu, baadhi ya nchi hizo ni Zambia, Ethiopia, Senegal, Ghana n.k.
Kampuni yake ya Dangote Cement imewekeza Dola 5 bilioni za Marekani katika kujenga viwanda vya saruji barani Afrika.
Waafrika tunaweza
Mnigeria huyu ni miongoni mwa Waafrika wanaoondoa fikra ya neno ‘mwekezaji’ lazima atoke Amerika, China, Ulaya na nchi nyingine, lakini siyo Afrika.
Wakati Dangote akifanya hayo, hivi karibuni Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo ya Biashara (Unctad) lilitoa ripoti inayoonyesha kwamba uwekezaji wa moja kwa moja kutoka nje (FDI) katika Bara la Afrika, umongezeka kwa asilimia 5.
Taasisi nyingine ya Kimataifa ya Ernest & Young inayojihusisha na ukaguzi wa mahesabu, kodi na ushauri kwa kampuni, yenye makao yake makuu jijini London Uingereza inasema wawekezaji wa Kiafrika wanaowekeza Afrika imeongezeka kutoka watu 27 mwaka 2003 hadi 145 mwaka 2011 sawa na asilimia 17 ya wawekezaji wote wa kigeni uliofanyika mwaka uliopita.
Utafiti huo unaonyesha kuwa miradi ya uwekezaji ya Waafrika wenyewe katika Bara la Afrika, imeongezeka kutoka miradi 339 mwaka 2003 hadi 857 mwaka 2013 sawa na asilimia 153.
Ernest & Young pia wanasema Benki za Nigeria na Kenya ni mifano halisi ya uwekezaji unaofanywa wawekezaji wa Afrika na imetoa mfano pia kwa Benki ya United Bank of Africa (UBA) ya Nigeria ambayo imewekeza katika nchi 18 barani Afrika ikiwamo Tanzania.
Utafiti wa Ernest & Young unasema ongezeko la Waafrika wanaowekeza barani humu ni dalili ya kujiamini kwamba Waafrika wanaweza shughuli za uwekezaji.

Jaji Mkuu Mstaafu kutoa ushahidi jaribio la kumtapeli Willbrod Slaa
 Hai. Jaji Mkuu Mstaafu,Barnabas Samatta ni miongoni mwa mashahidi 12 watakaotoa ushahidi katika kesi ya jinai ya jaribio la kumtapeli Katibu Mkuu wa Chadema,Dk Willbrod Slaa.
Wengine watakaotoa ushahidi katika kesi hiyo inayomkabili Abedi Adam Abedi (22) ni Dk Slaa mwenyewe na Mbunge wa Arusha Mjini kwa tiketi ya Chadema, Godbless Lema.
Orodha ya majina ya mashahidi hao ilitolewa mahakamani juzi mbele ya Hakimu Mkazi wa Wilaya ya Hai, Denis Mpelembwa na Mwendesha Mashtaka wa Takukuru, Maghela Ndimbo.
Wengine watakaotoa ushahidi ni wakili mashuhuri wa Chadema, Profesa Abdalah Safari, Rumisha Slaa, Happynes Masue, Godfrid Njau, Gervas Geneya, Neema Godbless,Aron Misanga, Prosper Mbilinyi na Judith Mashashi.
Akisoma maelezo ya awali, Ndimbo alidai kuwa kati ya Aprili na Mei, 2012, mshtakiwa alijitambulisha kwa Dk Slaa, Lema na Profesa Safari kuwa yeye ni mtumishi wa Takukuru.
Ilidaiwa kuwa katika kipindi hicho, mshtakiwa aliwapigia simu Dk Slaa, Lema na Profesa Safari na kujitambulisha kuwa yeye ni Abel Kibaso Mkuu wa Takukuru Wilaya ya Ulanga.
Katika kipindi hicho pia, mshtakiwa aliwapigia simu viongozi hao akijitambulisha ni Jaji mstaafu Samatta akitaka wampe pesa ili washinde katika kesi iliyokuwa mahakama ya Rufaa.
Rufaa hiyo namba 47/2012 ilifunguliwa na Lema dhidi ya Mussa Hamisi na wenzake akipinga hukumu ya Mahakama Kuu Arusha ya kupinga kuvuliwa Ubunge wa Arusha mjini kesi ambayo kwa sasa ilishatolewa uamuzi.
mashtaka huyo alidai mahakamani kuwa mshtakiwa alijifanya ni Jaji Mkuu Mstaafu Samatta wakati akijua siyo Jaji Samatta kwa lengo tu la kujipatia fedha kinyume cha sheria.
Hata hivyo Lema alishinda Rufaa hiyo na kurudishiwa Ubunge wake.
Mshtakiwa amekanusha mashtaka hayo na kesi hiyo imepangwa kuanza kusikilizwa rasmi Septemba 25 ambapo Jaji Samatta ni miongoni mwa mashahidi wa upande wa Jamhuri.


No comments: